• Nairobi
  • Last Updated May 8th, 2024 12:43 PM
Ramos aonyeshwa kadi nyekundu PSG wakikabwa koo na Lorient ligini

Ramos aonyeshwa kadi nyekundu PSG wakikabwa koo na Lorient ligini

Na MASHIRIKA

MAURO Icardi aliwaokolea waajiri wake Paris Saint-Germain (PSG) alama moja muhimu dhidi ya Lorient katika mechi ya Ligi Kuu ya Ufaransa (Ligue 1) mnamo Jumatano usiku.

Icardi alifunga bao mwishoni mwa kipindi cha pili kupitia kichwa baada ya kukamilisha krosi kutoka kwa Achraf Hakimi. Goli hilo lilipatikana dakika chache baada ya beki Sergio Ramos wa PSG kufurushwa uwanjani kwa kadi ya pili ya manjano. Lorient ambao kwa sasa wanashikilia nafasi ya 19 kwenye msimamo wa jedwali walifungiwa bao na Thomas Monconduit katika kipindi cha kwanza.

PSG walipoteza nafasi nzuri ya kupachika wavuni bao la pili na la ushindi kupitia kwa Angel di Maria aliyeshindwa kumzidi ujanja Paul Nardi sekunde chache kabla ya kipenga cha kuashiria mwisho wa mchezo kupulizwa. Mechi hiyo ilikuwa ya pili kwa Ramos kuchezea PSG tangu abanduke Real Madrid na kutua Ufaransa mwishoni mwa msimu wa 2020-21.

Kadi nyekundu aliyoonyeshwa katika mchuano huo dhidi ya Lorient ilikuwa yake ya 27 katika soka ya kitaaluma. Ramos aliyetokea benchi katika kipindi cha pili, alionyeshwa kadi ya kwanza ya manjano katika dakika ya 81 kabla ya kuonyeshwa ya pili dakika tano baadaye.

Ilikuwa mara ya tano katika mechi 19 za Ligue 1 msimu huu kwa PSG ya kocha Mauricio Pochettino kutoshinda mechi. Hata hivyo, wangali kileleni mwa jedwali la Ligue 1 kwa alama 46 huku pengo la pointi 13 likitamalaki kati yao na Nice wanaoshikilia nafasi ya pili.

MATOKEO YA LIGUE 1 (Jumatano):

Lorient 1-1 PSG

Bordeaux 2-3 Lille

Lyon 1-1 Metz

Marseille 1-1 Reims

Monaco 2-1 Rennes

Montpellier 4-1 Angers

Nice 2-1 Lens

St-Etienne 0-1 Nantes

Troyes 1-1 Brest

You can share this post!

Real wazamisha Bilbao na kufungua mwanya kileleni mwa La...

Man-City wakubali kuuzia Barcelona kiungo mvamizi Ferran...

T L