NA WANDERI KAMAU
GAVANA wa Murang’a Irungu Kang’ata amesema kuwa Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta alipoteza udhibiti wa kisiasa wa eneo la Mlima Kenya kwa kukosa “kuzingatia maonyo yaliyokuwa kwenye barua aliyomwandikia mnamo 2021”.
Mnamo Alhamisi, Dkt Kang’ata alisema kuwa Bw Kenyatta bado angekuwa na ushawishi wa kisiasa katika ukanda huo ikiwa angefuata tahadhari alizompa, badala ya kumwadhibu.
“Imani yangu ni kwamba, ikiwa Bw Kenyatta angefuata yale niliyomwambia, hangekuwa katika mahali alipo kisiasa sasa. Mimi nilikuwa tu kama nabii. Nilimwasilishia tu ujumbe kuhusu hali niliyoiona miongoni mwa wenyeji wa Mlima Kenya. Badala ya kuzingatia yale yaliyokuwa kwenye barua hiyo, serikali yake iliamua kunihangaisha,” akasema Dkt Kang’ata kwenye mahojiano na kituo kimoja cha redio.
Gavana huyo alirejelea simulizi kadhaa kwenye Biblia, zinazoeleza madhara yaliyowakumba wafalme waliokosa kuzingatia maonyo waliyopewa na watu waliotumwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
“Tangu zamani, mwenye ujumbe huwa haingiliwi wala kushambuliwa kwa namna yoyote ile. Hayo ndiyo mafunzo tuliyopewa na mababu zetu. Jamii na viongozi waliokuwepo walikuwa wakizingatia ujumbe walioletewa. Mimi nilielekezewa vitisho vya kila aina, licha ya kuwa mtumwa kuhusu hali ya kisiasa iliyokuwepo wakati huo,” akasema gavana huyo.
Kutokana na barua hiyo, Dkt Kang’ata alinyang’anywa nafasi ya Kiranja wa Wengi katika Seneti, aliyokuwa akiishikilia wakati huo.