• Nairobi
  • Last Updated May 7th, 2024 9:48 PM
Mjukuu wa Moi akubali watoto aliokana awali

Mjukuu wa Moi akubali watoto aliokana awali

Na JOSEPH OPENDA

MJUKUU wa aliyekuwa rais, Mzee Daniel Moi hatimaye amekubali kuwajibikia malezi ya watoto wawili anaoshutumiwa kuwatelekeza baada ya uchunguzi wa DNA kuthibitisha kwamba, ndiye baba mzazi.

Bw Collins Kibet Moi alieleza Mahakama ya Nakuru kwamba, yupo tayari kuchangia kwenye malezi ya watoto hao wawili aliowazaa na Bi Gladys Jeruto Tagi, kabla ya wao kutengana zaidi ya miaka minane iliyopita.

Alisema anadhamiria kuwasilisha mapendekezo rasmi mbele ya korti pamoja na Bi Tagi kuhusu jinsi atakavyowashughulikia watoto hao.

Bw Kibet, aliyekuwa amekanusha kuwazaa watoto hao, alilazimika kunyenyekea baada ya uchunguzi huo kufichua kuwa, ndiye baba mzazi wa watoto hao wenye umri wa miaka 11 na miaka tisa.

Kulingana na ripoti ya DNA, matokeo ya vipimo yaliyowasilishwa kortini mnamo Agosti 25, yalionyesha kuwa chembechembe za DNA za Bw Kibet zinafanana na za watoto hao wawili kwa asilimia 99.9, kumaanisha uwezekano wa kiwango cha juu zaidi kuwa ndiye baba mzazi wa watoto hao.

Akiwa mbele ya Hakimu Mkuu Benjamin Limo, Bw Kibet, kupitia wakili wake aliomba muda zaidi ili kuwasilisha mapendekezo yake kuhusu mchango wake katika malezi.

“Mshtakiwa amekubali kuwasaidia watoto lakini hana uwezo wa kulipa kiasi cha pesa kilichoitishwa na mlalamishi. Hivyo basi, anaomba idhini ya korti kuwasilisha mapendekezo rasmi kuhusu jinsi atakavyowasaidia watoto hao,” alisema wakili.

Bi Tagi aliyewasilisha kesi hiyo mnamo Machi alikuwa ameitisha Sh1 milioni kugharamia malezi ya watoto.Kupitia wakili wake David Mong’eri, mama huyo alidai pesa hizo ni za kugharamia mahitaji ya kibinafsi ya watoto hao.

You can share this post!

Vihiga Queens wajikatia tiketi ya kulimana na Simba Queens

Amani: Museveni aombwa atumie busara Sudan Kusini