NA WINNIE ONYANDO
VUGUVUGU la Bunge la Mwananchi sasa linataka leseni ya huduma za Shirika la Ndege la Syward ifutiliwe mbali likilalamikia usalama abiria kutotiliwa maanani.
Kulingana na mwenyekiti wa vuguvugu hilo, Frank Awino, huduma zinazotolewa na shirika hilo ni hatari kwa usalama wa wateja.
“Tunataka leseni ya oparesheni ya shirika la Syward ifutiliwe mbali kwa sababu inatoa huduma ambazo ni hatari kwa wasafiri,” akasema Bw Awino.
Shirika hilo linalotoa huduma za usafiri kwa wateja wanaosafiri Kakamega, Kitale, Mombasa, Lamu, Eldoret, Diani, Lodwar na Malindi linaongozwa na Muhumedn Abdi Mohammed.
Kando na hayo, Bw Awino alidai kuwa tikiti ya usafiri inayotolewa na shirika hilo ni ghali kushinda mashirika mengine ya ndege.
“Tunaamini kwamba shirika hilo halifai kutoa huduma za usafiri kufuatia masuala tuliyoainisha,”
Kutokana na hilo, vuguvugu hilo limewasilisha kesi mahakamani.
Aidha, kesi hiyo iliyowasilishwa makahamani imeorodheshwa kama nambari E441 ya 2023.
Bw Awino alisema kuwa kuna haja Mamlaka ya Usimamizi wa Viwanja vya Ndege Nchini kupiga marufuku shirika hilo dhidi ya kutoa huduma nchini.
“Ikiwa hilo halitafanyika, wanabunge wataandaa maandamano,” akaonya Bw Awino.