• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 10:09 AM
Waliotia ‘mchele’ kwa pombe ya mteja wakamatwa

Waliotia ‘mchele’ kwa pombe ya mteja wakamatwa

Na GEORGE MUNENE

WANAWAKE wawili wanaodaiwa kumpumbaza mwanaume kisha kumwibia pesa baada ya kumtilia ‘mchele’ kwenye pombe yake, jana walikamatwa na polisi katika Kaunti ya Kirinyaga.

Wawili hao wanashukiwa kuwa kati ya genge la warembo ambao wamekuwa wakiwawekea dawa ya kuwapotezea fahamu kwenye kinywaji na kuwaibia. Walinaswa kutoka kwa maficho yao na wanaendelea kuzuiwa katika kituo cha polisi cha Wang’uru wanakohojiwa kuhusu tukio hilo.

Mkuu wa Polisi wa Mwea Mashariki Daniel Kitavi alieleza Taifa Leo kwamba, mwanaume aliyeibiwa bado hajapata fahamu na amelezwa katika hospitali ya misheni ya Mwea akiwa katika hali mahututi.

Kwa mujibu wa shahidi, mwanaume huyo aliingia kwenye baa moja maarufu mjini Ngurubani na akaagiza bia. Baada ya muda mchache wanawake hao wawili walifika kisha wakaomba wajumuike naye mezani.

Walipoendelea kunywa, mwanaume huyo alienda haja na hapo ndipo wanawake hao wakamtilia dawa katika kinywaji chake. Bila ufahamu wowote, alirejea kunywa kisha akapoteza fahamu na wanawake hao wakampora pesa, kadi yake ya ATM, kitambulisho na mali nyingine.

Mwanaume huyo aliokolewa na wasamaria wema ambao walimfikisha hospitalini baada ya kumpata hajijui hajitambui sakafuni.

“Hakuweza kuongea au kusimama. Nafikiri alikuwa amebururwa sakafuni baada ya kuibiwa,” akasema shahidi mwingine ambaye alikataa kufichua jina lake.

Polisi walipata vidokezo na kuvamia chumba moja ambako wanawake hao walikuwa wamejificha na kuwakamata na kupata baadhi ya dawa zinazodaiwa zilitumika.

You can share this post!

MUUNGANO WA RAILA, RUTO WAINGIA DOA

Zakat Kenya kuwafaa Waislamu Ramadhan