• Nairobi
  • Last Updated May 6th, 2024 8:55 PM
Agizo la Joho kuhusu miraa lapingwa vikali

Agizo la Joho kuhusu miraa lapingwa vikali

Na WACHIRA MWANGI

SERIKALI ya Kaunti ya Mombasa, italazimika kutafuta pesa kwingine baada ya Gavana Hassan Joho kuagiza kuwa magari ya kusafirisha miraa yasitozwe kodi.

Miraa na muguka ni miongoni mwa bidhaa zinazotozwa kiasi kikubwa zaidi cha kodi za usafirishaji kuingia Mombasa, miongoni mwa mazao ya kilimo.

Kulingana na Sheria ya Fedha ya 2021/22 iliyopitishwa na Bunge la Kaunti ya Mombasa, kiasi kidogo zaidi cha kodi ya kusafirisha miraa ni Sh5,000 kwa mkokoteni huku kiasi cha juu zaidi kikiwa Sh50,000 kwa malori na mabasi yanayozidi tani saba.

Bw Joho akiwa katika mkutano wa kisiasa Kaunti ya Meru ambapo aliandamana na Kiongozi wa ODM Raila Odinga mnamo Jumatatu, aliambia wakazi wa eneo hilo kwamba ameagiza kodi hizo ziondolewe ili kuwasaidia kiriziki.

Waziri wa Fedha katika Kaunti ya Mombasa, Bi Mariam Mbaruk, Jumanne alisema maafisa wa kaunti watatii agizo hilo.

“Hayo ni maagizo kutoka kwa Gavana kwa hivyo tayari tumeanza kuyatekeleza. Tuliacha kutoza kodi kwa miraa zinazoingia Mombasa tangu juzi (Jumatatu),” akasema Bi Mbaruk.

Haikubainika mara moja kama sheria zozote za fedha zilifanyiwa marekebisho kabla agizo hilo la Bw Joho kuanza kutekelezwa.

Wasiwasi

Kando na athari za agizo hilo kwa ukusanyaji wa kodi katika kaunti, baadhi ya mashirika yameeleza wasiwasi kwamba litasababisha ongezeko la bidhaa hiyo ambayo imekuwa ikilaumiwa kwa athari za afya na kijamii.

“Hili ni pigo kiuchumi na hakufaa kutoa agizo aina hiyo. Kodi hizo hutegemewa kutekeleza miradi kwa manufaa ya wakazi. Pia kuna changamoto nyingi za kiafya zinazosababishwa na matumizi ya miraa na muguka,” Mkurugenzi Mkuu wa shirika la Reachout Centre akasema.

Afisa Mkuu Mtendaji wa Shirika la Kitaifa la Kukabili Uraibu wa Dawa za Kulevya (Nacada), Bw Victor Okioma, alitofautiana na wanasiasa wanaosema kuwa miraa haina madhara ya kiafya.

“Tumehamasisha umma kuhusu madhara ya miraa, na chaguo ni lao. Sawa na pombe, huwa tunatoa ilani kwa kuzingatia utafiti wa kisayansi. Uraibu wa miraa huathiri uwezo wa mtu kimwili, kiakili na hata kiuchumi,” akasema Bw Okioma.

Mshirika wa Bodi ya Nacada, Bi Farida Seif, alikosoa uamuzi wa kaunti kuondoa kodi ya kusafirisha miraa na kusema utasababisha ongezeko la matumizi yake.

“Tumekuwa tukifanya mashauriano na maafisa wa afya na wa kaunti ili kutafuta jinsi miraa na muguka inavyoweza kupigwa marufuku katika kaunti. Hii ni hasara kwa uchumi na afya ya watu wetu,” akasema Bi Farida.

Miraa imeorodheshwa kama dawa ya kulevya na Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO), na matumizi yake yalipigwa marufuku katika baadhi ya mataifa ya Ulaya.Kulingana na utafiti, matumizi ya miraa kwa muda mrefu huweza kusababisha meno kuoza na pia kuangamiza hamu ya mraibu kushiriki tendo la ndoa.

You can share this post!

Korti yaelezwa jinsi mwanamke alivyoibia mfanyabiashara

Hofu ya siasa za urithi kutawala Mashujaa Dei

T L