• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 1:22 PM
Mbunge asema aliolewa akiwa kimwana bikira

Mbunge asema aliolewa akiwa kimwana bikira

NA CHARLES WASONGA

MBUNGE Mwakilishi wa Kike wa Kaunti ya Kisii Dorice Donya, Jumatano, Mei 3, 2023, ameibua kicheko bungeni alipodai kuwa aliolewa akiwa bikira.

Bi Donya alikuwa akiomboleza kifo cha Mama Agnes Moraa, mamake Mbunge Mwakilishi wa Kike wa Kaunti ya Nyamira Jerusha Momanyi, alipotoa madai hayo kwenye kikao cha alasiri.

Ufichuzi wake uliibua kicheko miongoni mwa wabunge wa mirengo yote bungeni.

Bi Donya alisema alikutana na mama Moraa mara kadha alipokuwa akifanya kazi kama mtangazaji wa Egesa FM inayopeperusha matangazo kwa lugha ya Ekegusii.

“Nyakati zote Mama Moraa alielekeza wasichana wadogo ipasavyo. Mama alihimiza ndoa ya harusi. Alihimiza kwamba wasichana waolewe katika umri mzuri na wakiwa bikira,” Bi Donya akasema.

“Donya anayesimama mbele yenu hapa alitii kanuni ya kuwa bikira. Niliolewa nikiwa ningali bikira,” Mbunge huyo akaongeza.

Bi Donya aliongeza kuwa Mama Agnes alikuwa mstari wa mbele kupambana na kero ya wasichana kutungwa mimba wakiwa wadogo katika jamii yake.

Mbunge huyo Mwakilishi wa Kisii alisema yeye ni mama wa wasichana wawili, ambao pia alisema kuwa wataolewa wakiwa mabikira.

“Mjue kuwa wasichana wangu watakuwa mabikira watakapokuwa wakiolewa, kwa heshima ya Mama Agnes,” Bi Donya akaeleza.

Naye Bi Momanyi alisema mamake alikuwa mfano bora kwa wanawake katika jamii ya Ekegusii, haswa kwa kuwatia shime wajiunge na biashara.

Mbunge huyo Mwakilishi wa Kaunti ya Nyamira alisema kumbukumbu ya mamake zitaendelea kuvipa shime vizazi vijavyo.

  • Tags

You can share this post!

Fraser-Pryce, Mkenya Imali kukabiliana Kip Keino Classic

Azimio wasitisha maandamano baada ya Kenya Kwanza kumwondoa...

T L