• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 6:07 PM
Eric Omondi ashauriwa ajihusishe kikamilifu na majukumu ya ulezi

Eric Omondi ashauriwa ajihusishe kikamilifu na majukumu ya ulezi

Na WANGU KANURI

MKURUGENZI mkuu wa kampuni ya usafiri ya Bonfire, Bi Sarah Kabu amemshutumu mcheshi Eric Omondi baada ya kudaiwa kutoshughulika na malezi ya mwana wake Zahari.

Eric Omondi na Jacque Maribe ni wazazi wa mtoto Zahari.

Tukio hilo linajiri baada ya Omondi kufichua kuwa alimtunga mimba Bi Picasah ambaye anafahamika kama Miss P. Isitoshe, Omondi alieleza kuwa atawajibika na malezi ya mtoto huyo.

“Nilikutana na mwanamke huyu mrembo miezi tano iliyopita katika sherehe moja na nimemuahidi kuwajibika katika kila kitu. Watoto ni baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu,” aliandika Omondi baada ya kuposti picha na Miss P.

Maribe aliyeonekana kukerwa na ujumbe huo aliuliza kwa kinaya, “Kuwajibika? @catewamaribe kuja uzungumzie haya kwani siwezi. Miaka saba ya kuwajibika?”

Bi Kabu kwa upande wake alimsikitikia Bi Maribe huku akimweleza Bw Omondi ajishughulishe na malezi ya mtoto huyo wake.

“Eric wewe ni rafiki yangu mzuri na mimi ni shabiki wako mkubwa lakini kutolipa karo ya shule na kutokidhi mahitaji mengine ya mtoto wako, kisha kufanya utani mtandaoni hilo si jambo la kuchekesha. Ninasikitikia Jacque. Jasirika kama mwanamume na uwajibike kikamilifu. Ninajua unatengeneza pesa nzuri kupitia ucheshi wako. Maisha ni magumu,” akasema.

Maribe kwa upande wake ameshikilia kuwa Eric hashughuliki na malezi ya mtoto wao Zahari.

“Kwa kweli ninampenda mtoto huyu wangu, tunda nililotaka toka tumbo langu la uzazi. Nimebarikiwa kuwa mlezi wake.

“Watu wengi wamenieleza nisizungumzie ukweli halisia wa matukio na ninaheshimu uamuzi huo. Hata hivyo, ninawaomba mniheshimu ninapoelezea yaliyo kweli. Siwezi anika mambo mabaya mtandaoni.

“Wengi wa marafiki wangu wa kweli wanampenda Zahari na hata wazazi wangu wanamuenzi sana. Mimi ndiye mzazi pekee kwa mtoto Zahari na ninafanya kila kitu peke yangu. Lengo langu ni kuhakikisha kuwa amekua mtu bora kama alivyo sasa. Ninampenda mtoto wangu na nitasimama naye kila siku,” akasema Bi Maribe.

Mwanahabari Maribe anayehusishwa na kesi ya mauaji, alimfichua baba ya mtoto wake mnamo 2019.

Kwake Maribe, mtoto Zahari ni baraka kwani alimpata baada ya matatizo ya muda ya kushika mimba.

Hapo awali kwenye mahojiano, Maribe alifichua kuwa walikuwa marafiki wa karibu sana na Eric kwa miaka nusura tano kabla hawajaamua kuwa kwenye mahusiano ya kimapenzi.

“Wakati niligundua nina mimba, nilifurahi sana kwani nilikuwa nataka sana mtoto licha ya matatizo. Eric kwa upande wake hakuwa na uhakika kuhusu kutaka mtoto sababu ya kazi zake,” akaeleza.

Hata hivyo, panda-shuka za mahusiano ziliwafanya watengane na wakauvunja uhusiano wao.

Fauka ya hayo, Maribe aliwahi kiri kuwa anahusiana tu na Omondi katika malezi ya mwanao na hanui kuchumbiana naye tena.

You can share this post!

WANGARI: Kongamano kuu la mazingira lizindue viongozi...

Daraja la kuunganisha Murera na Kalimoni lazinduliwa

T L