• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 7:50 AM
Chelsea waaibisha Southampton kwa kichapo cha 6-0 katika EPL ugani St Mary’s

Chelsea waaibisha Southampton kwa kichapo cha 6-0 katika EPL ugani St Mary’s

Na MASHIRIKA

CHELSEA waliweka kando maruerue ya kuchapwa 3-1 na Real Madrid katika mkondo wa kwanza wa robo-fainali ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) kwa kuponda Southampton 6-0 katika mechi ya Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) mnamo Jumamosi ugani St Mary’s.

Chelsea walishuka dimbani wakiwa pia na hasira ya kujinyanyua ligini baada ya limbukeni Brentford kuwatandika 4-1 katika mechi ya awali uwanjani Stamford Bridge.

Sasa ushindi mnono dhidi ya Southampton yanatarajiwa kuwapa motisha zaidi ya kubatilisha matokeo ya mkondo wa kwanza dhidi ya Atletico watakaowaalika kwa marudiano mnamo Aprili 12, 2022 uwanjani Wanda Metropolitano, Uhispania.

Fowadi Timo Werner wa Chelsea walishuhudia makombora yake mawili yakigonga mwamba wa goli la Southampton chini ya dakika saba za ufunguzi wa mchezo kabla ya Marcos Alonso kufungulia waajiri wake ukurasa wa mabao kupitia krosi ya Mason Mount.

Mount alifunga bao la pili la Chelsea katika dakika ya 16 kabla ya Werner kumwacha hoi kipa Fraser Forster dakika sita baadaye. Werner aliyefunga bao jingine mwanzoni mwa kipindi cha pili alikomesha ukame wa magoli tangu acheke na nyavu za wapinzani ligini miezi sita iliyopita. Goli hilo lilikuwa dhidi ya Southampton mnamo Oktoba 2021.

Bao jingine la Chelsea waliokosa huduma za fowadi Romelu Lukaku na nahodha Cesar Azpilicueta lilifumwa kimiani na Kai Havertz.

Baada ya kurudiana na Real ugani Bernabeu, Chelsea wameratibiwa kuvaana na Crystal Palace katika nusu-fainali ya Kombe la FA mnamo Aprili 16, 2022 ugani Wembley.

Chelsea kwa sasa wanakamata nafasi ya tatu kwenye msimamo wa jedwali la EPL kwa alama 62, tano kuliko Tottenham Hotspur wanaofunga mduara wa nne-bora.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Saudia kuruhusu mahujaji milioni 1

Brighton yadidimiza matumaini ya Arsenal kumaliza msimu wa...

T L