• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 11:13 AM
Mount afunga mabao matatu na kuongoza Chelsea kukomoa Norwich 7-0 katika EPL

Mount afunga mabao matatu na kuongoza Chelsea kukomoa Norwich 7-0 katika EPL

Na MASHIRIKA

MASON Mount alipachika wavuni mabao matatu na kuongoza Chelsea kupepeta Norwich City 7-0 uwanjani Stamford Bridge.

Chini ya kocha Thomas Tuchel, Chelsea walifunga mabao mawili chini ya dakika 18 za kipindi cha kwanza kupitia Mount na Callum Hudon-Odoi. Ilikuwa mara ya kwanza kwa wawili hao kufunga wakichezea Chelsea muhula huu.

Ushirikiano mkubwa kati ya Mount na Hudson-Odoi ulichangia bao la tatu ambalo Chelsea walifungiwa na Reece James kabla ya kipenga cha kuashiria mwisho wa kipindi cha kwanza kupulizwa.

Beki Ben Chilwell alicheka na nyavu za wapinzani kwa mara ya nne mfululizo akivalia jezi za Chelsea msimu huu na kufanya mambo kuwa 4-0 kunako dakika ya 57.

Mbali na Max Aarons wa Norwich aliyejifunga kunako dakika ya 62, mabao mengine ya Chelsea yalijazwa kimiani kupitia Mount katika dakika za 85 na 90 mtawalia.

Norwich walikamilisha mchuano huo wakiwa na wachezaji 10 pekee uwanjani baada ya difenda Ben Gibson kuonyeshwa kadi nyekundu katika dakika ya 65.

Kutokuwepo kwa washambuliaji Romelu Lukaku na Timo Werner waliojeruhiwa wakati wa mechi ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) dhidi ya Malmo mnamo Oktoba 20, kulimpa Tuchel katika ulazima wa kuchezesha Kai Havertz kama fowadi mkuu huku akipigwa jeki na Mount pamoja na Hudson-Odoi.

Chelsea kwa sasa wanaselelea kileleni mwa jedwali la EPL kwa pointi 22 huku Norwich wakivuta mkia kwa alama mbili kutokana na mechi tisa zilizopita ligini.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Ruto awarai vijana kutotumiwa kuzua ghasia

TAHARIRI: CBC ikitekelezwa vizuri spoti itakua

T L