• Nairobi
  • Last Updated May 6th, 2024 8:55 PM
Red Devils wamnyaka Martinez wa Ajax

Red Devils wamnyaka Martinez wa Ajax

NA MASHIRIKA

BEKI Lisandro Martinez, 24, anatarajiwa kupiga jeki safu ya ulinzi ya Manchester United baada ya kuagana na Ajax ya Ligi Kuu Uholanzi (Eredivisie).

Martinez atatua ugani Old Trafford kwa ada ya Sh6.9 bilioni mwanzoni, ambayo itaongezeka hadi Sh8 bilioni.

Beki huyo, aliyekuwa pia akiwaniwa na Arsenal, atavalia jezi ya Man-United kwa miaka mitano ijayo huku akitia mfukoni mshahara wa Sh17 milioni kwa wiki.

Ujira huo ni sawa na ule ambao Victor Lindelof na Fred Paula Santos wanadumishwa ugani Old Trafford.

Kwa mujibu wa maelewano, mabingwa hao mara 20 wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) watakuwa huru kurefusha kandarasi ya Martinez kwa miezi 12 kutegemea matokeo yake.

Martinez amesakatia Ajax mara 120 tangu abanduke kambini mwa Defensa y Justica ya Argentina kwa kitita cha Sh888 milioni mnamo 2019.

Amewahi pia kuchezea Newell’s Old Boys ya Argentina baada ya kupokea malezi ya soka kambini mwa Club Urquiza (2002-06) na Club Libertad (2006-2014).

Sogora huyo amechezea Argentina mara saba tangu mabingwa hao mara mbili wa Kombe la Dunia (1986, 1978) wamwajibishe kwa mara ya kwanza mnamo Machi 2019.

Anakuwa mchezaji wa tatu kuingia katika sajili rasmi ya Man-United muhula huu baada ya beki Tyrell Malacia aliyetokea Feyenoord ya Uholanzi kwa Sh2.2 bilioni na kiungo Christian Eriksen aliyetua Old Trafford bila ada yoyote.

Mkataba wa Martinez na Ajax ulikuwa utamatike Juni 2025. Sasa ataungana na kocha mpya wa Man-United, Erik ten Hag, aliyewahi kumnoa kambini mwa Ajax kuanzia 2019.

Chini ya Ten Hag, Martinez alisaidia Ajax kunyanyua taji la Eredivisie mnamo 2021 na 2021 huku akizolea miamba hao ufalme wa Dutch Cup mnamo 2021.

Mchango wake mkubwa ulimfanya kutawazwa Mchezaji Bora wa Mwaka klabuni Ajax mnamo 2021-22.

Ten Hag bado analenga wachezaji zaidi jinsi anavyozidi kukisuka upya kikosi chake cha Man-United,.

Mkufunzi huyo sasa anahemea maarifa ya kiungo wa zamani wa Ajax, Frenkie de Jong, aliye kambini mwa Vigogo wa Ligi Kuu ya Uhispania (La Liga), Barcelona.

  • Tags

You can share this post!

Korir avunia Kenya fedha marathon ya dunia nchini USA

Arsenal waafikiana na Man-City kuhusu uhamisho wa Oleksandr...

T L