NA SAMMY WAWERU
MBUNGE wa Tiaty William Kamket ametangaza kushirikiana na kambi ya Kenya Kwanza, inayoongozwa na Dkt William Ruto.
Kwenye uchaguzi mkuu wa Agosti 9, 2022, Dkt Ruto aliwania urais kupitia chama cha United Democratic Alliance (UDA) na baada ya kura kujumlishwa, alitangazwa mshindi na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) Wafula Chebukati.
Ushindi wake hata hivyo umepingwa na kinara wa Azimio la Umoja-One Kenya, Raila Odinga ambapo kesi hiyo kwa sasa inaendelea kusikilizwa katika Mahakama ya Upeo.
Ruto kupitia kurasa zake za mitandao ya kijamii Alhamisi, alitangaza hatua ya Bw Kamket kushirikiana na Kenya Kwanza.
“Kufanya kazi kwa pamoja ni muhimu kuafikia malengo tuliyoahidi Wakenya. Ninaridhia kumkaribisha mbunge wa Taity, William Kamket katika muungano wa Kenya Kenya,” Ruto akaandika, chapisho ambalo liliandamana na picha za wawili hao wakiwa pamoja katika makao yake makuu Karen, Nairobi.
Katika uchaguzi mkuu, Kamket alihifadhi kiti chake kupitia KANU – chama kinachoongozwa na aliyekuwa seneta wa Baringo, Gideon Moi.
Gideon ni mshirika wa Azimio la Umoja. Bw Kamket ni mwandani wa mwenyekiti huyo wa KANU.
Itakumbukwa kwamba mbunge huyo amekuwa mmoja wa wakosoaji wa Dkt Ruto, wakati akihudumu kama naibu wa rais katika serikali inayoondoka ya Jubilee.