NA JAMES MURIMI
KIONGOZI wa chama cha The Service Party (TSP), Mwangi Kiunjuri na Mbunge wa Laikipia Mashariki, Amin Deddy wameagizwa kufika mbele ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kwa madai ya kuzua fujo katika mkutano wa kisiasa mjini Nanyuki wiki jana.
Mkutano huo wa kampeni uliongozwa na Naibu Rais William Ruto anayewania urais kwa tiketi ya chama cha United Democratic Alliance (UDA).
Bw Deddy anataka kuhifadhi kiti chake kwa tiketi ya chama cha UDA huku Bw Kiunjuri akipania kutwaa kiti hicho kwa tiketi ya TSP.
Wawili hao ambao wanaegemea muungano wa Kenya Kwanza (KKA) walikuwa wamesafirisha wafuasi wao kutoka sehemu mbalimbali kwa ajili ya kutia presha waidhinishwe hadharani na Dkt Ruto.
Lakini saa mbili kabla ya kuwasili kwa Naibu Rais, makundi ya vijana wafuasi wa wanasiasa hao walizua fujo katika uwanja wa Nanyuki Central Park na kutisha kusambaratisha mkutano huo.
Polisi waliingilia kati na kuwakamata vijana watano wakiwa na silaha butu.
Hata hivyo, mkutano uliendelea baadaye bila fujo zozote.