MIKIMBIO YA SIASA: Juhudi za Raila kukomboa Jubilee zinaweza zisifaulu
NA CHARLES WASONGA
HITAJI la kisheria kwamba Rais Mstaafu sharti ajiuzulu nyadhifa za uongozi katika chama cha kisiasa au muungano wa vyama, miezi sita baada ya kuondoka afisi huenda likaponza juhudi za kukomboa Jubilee.
Aidha, hatua ya Rais William Ruto kuonekana kuteka asasi huru za serikali haswa zenye wajibu wa kusimamia mfumo wa utoaji haki itasambaratisha juhudi hizo zinazoendeshwa na Katibu Mkuu aliyesimamisha kazi Jeremiah Kioni kwa usaidizi wa kinara wa Azimio Raila Odinga.
Kwa mujibu wa sheria hiyo kuhusu malipo ya pensheni ya Rais, kando na kujiondoa wadhifa wa kiongozi wa Jubilee, Bw Uhuru Kenyatta pia atalazimika kujiondoa kama mwenyekiti wa Baraza Kuu la Azimio.
Kwa kuzingatia matakaa ya miezi sita yaliyowekwa na sheria hiyo, Bw Kenyatta atahitajika kujiondoa nyadhifa hizo mbili kufukia Machi 13, 2023, ikizingatiwa kuwa aliondoka afisini mnamo Septemba 13, 2022.
Lakini katika uamuzi wake majuma mawili yaliyopita Baraza Kuu la Kitaifa (NEC) ya Jubilee liliahidi kuandaa mkutano maalum wa kitaifa wa wajumbe (NDC) wa Jubilee ndani ya kipindi cha miezi sita.
Hii ina maana kuwa mkutano wa asasi hiyo yenye mamlaka makubwa zaidi katika chama chochote cha kisiasa, utafanyika baada ya Bw Kenyatta kung’atuka kama kiongozi wa chama cha Jubilee.
Wakati wa mkutano huo uliofanyika katika mkahawa mmoja mjini Naivasha Bw Kioni alitimuliwa sawa na naibu mwenyekiti David Murathe na Mweka Hazina wa Kitaifa Kagwe Gachohi.
Mwakilishi wa Kenya katika Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) Kanini Kega aliyeteuliwa kuwa kaimu Katiba Mkuu huku Mbunge wa Eldas Aden Keynan akiteuliwa kuwa Naibu Mwenyekiti. Naye Mbunge wa Kitui Kusini Rachel Nyamai aliteuliwa kuwa kaimu mwekahazina.
Mapinduzi hayo yalifanyika siku chache baada ya jumla ya wabunge 30 wa Jubilee kumtembelea Rais Ruto katika Ikulu ya Nairobi ambapo walijitenga na Azimio na kuahidi kuunga mkono sera za muungano tawala Kenya Kwanza ndani na nje ya Bunge.
Wanachama hao wa NEC wakiongozwa na mwenyekiti wa Jubilee Nelson Dzuya, pia waliahidi kuwa wanaazisha mchakato wa kuunda ushirikiano na Kenya Kwanza.
Siku chache baadaye, Msajili wa Vyama vya Kisiasa Anne Nderitu aliidhinisha mapinduzi hayo huku akisisitiza kuwa mkutano huo wa NEC ulikuwa halali na uliandaliwa kufungamana na Katiba ya Jubilee.
“Afisi yangu imepokea maamuzi ya baraza la NEC la Jubilee kufuatia mkutano uliofanyika mjini Naivasha. Mkutano huo uliitishwa kihalali na mwenyekiti wa Jubilee na kuendeshwa kulingana na Katiba ya chama hicho,” akasema kwenye barua kwa maafisa hao wapya wa chama.
Baadaye maafisa hao wapya wakiongozwa na Bw Kega walifululiza hadi katika makao makuu ya Jubilee mtaani Lavington, Nairobi na kutangaza kwa sasa wao ndio wameshika usukani.
“Aidha, kamati ya nidhamu ya chama imemwandikia maafisa waliotumuliwa wakitakiwa kufika mbele yake kujitetea inavyohitajika kisheria,” akasema Bw Kega ambaye ni Mbunge wa zamani wa Kieni.
Uwepo wa idadi kubwa wa maafisa wa polisi katika afisi hizo maafisa hao wapya walipokuwa wakiwahutubia wanahabari, ni kiashirio tosha kwamba mapinduzi katika Jubilee yanaungwa mkono na serikali.
Japo Bw Kioni na wenzake waliotimuliwa walipata afueni ya muda kufuatia hatua ya Jopo la Kutatua Mizozo ya Vyama vya Kisiasa (PPDT) kusitisha mapinduzi hayo hadi maombi ya walalishi yatakaposikizwa Februari 24, dalili zaonyesha kuwa hawatafaulu.
“Bw Kioni na wandani wake wa Azimio wakiongozwa na Raila waelewe kwamba Rais Ruto ameapa kutwaa Jubilee. Hii ndio maana afisi ya msajili wa vyama vya kisiasa imeidhinisha kutimuliwa kwake. Jopo la PPDT pia itatupilia mbali malalamishi ya Kioni kwa sababu asasi hiyo ni mojawapo ya asasi huru za serikali ambazo zimetekwa na serikali na sasa zinatekelezwa matakwa yake,” anasema mchanganuzi wa masuala ya kisiasa Martin Andati.
Anatoa mfano wa Afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (ODPP) ambayo tangu Rais Ruto alipoingia mamlakani imeondoa kesi zilizowakumba baadhi ya wandani wa kiongozi huyo wa kitaifa.
“Jubilee itatwaliwa na mrengo wa Kenya Kwanza kwa urahisi kwa sababu Uhuru anatarajiwa kiondoa kama kiongozi na hatakuwa na ushawishi wowote katika chama hicho hata akisalia kuwa mwanacha mwa kawaida,” anaongeza.
Next article
KIGODA CHA PWANI: Kaunti za Pwani zaweza kujikimu bila...