Na SHABAN MAKOKHA
GAVANA wa Kakamega, Wycliffe Oparanya amesema alijiondoa kwenye kinyang’anyiro cha urais baada ya Rais Uhuru Kenyatta kumshawishi amuunge mkono Kinara wa ODM, Raila Odinga.
Alisema kuwa alijiondoa hata baada ya kulipa ada ya uteuzi iliyotozwa na chama cha ODM.
“Baada ya kulipa ada ya Sh1 milioni, sikupata habari yoyote ama barua kutoka kwa chama hicho,” akasema Bw Oparanya.
Alisema kuwa baadaye alipata ujumbe kutoka kwa Rais Kenyatta.
“Baada ya kutangaza azma yangu ya kuwania kiti cha urais, nilipokea simu kutoka Ikulu ikinikaribisha kukutana na Rais Kenyatta Mombasa. Nilipoenda Mombasa State Lodge, nilikutana na Rais Kenyatta akiwa ameketi peke yake akinisubiri,” akadokeza.
“Rais alinishawishi nijiondoe kwenye kinyang’anyiro cha urais ili nimuunge mkono Bw Odinga ambaye alisema ndiye mgombea wa kiti hicho aliyemteua.”