• Nairobi
  • Last Updated May 7th, 2024 9:48 PM
Bunge lasitisha shughuli Uganda kufuatia milipuko ya mabomu

Bunge lasitisha shughuli Uganda kufuatia milipuko ya mabomu

Na FRANLIN DRAKU, Mwandishi wa NMG

KAMPALA, Uganda

BUNGE la Uganda limesitisha, kwa muda, shughuli zake baada ya milipuko miwili ya mabomu kutokea Jumanne asubuhi jijini Kampala.

Naibu Spika wa bunge hilo Anita Among, aliwaagiza wabunge kusalia nyumbani kwa muda usiojulikana ili kutoka nafasi kwa uchunguzi kuhusu matukio hayo.

Mlipuko wa kwanza ulitokea karibu na jengo moja katikati mwa jiji hilo.

Dakika chache baadaye, mlipuko mwingine ukatokea katika barabara ya Parliament Avenue.

Jumba la Jubilee Insurance ambako kuna afisi za Inspekta Jenerali wa Afisi za Serikali liliathiriwa na mlipuko huo.

Mlipuko wa kwanza ulitokea katika na jumba la Kooki Tower, mkabala na kituo cha Polisi cha Central.

“Bunge limefungwa na wabunge wanashauriwa kutofika hapa, ila wasalie nyumbani,” Bi Among akasema.

Naibu huyo wa Spika alifafanua kuwa shughuli zote za bunge hilo zimesitishwa ikiwemo mikutano ya kamati zake; ya ana kwa ana au kupitia mitandaoni.

Maafisa wa polisi pia waliziba barabara zote za kuingia na kuondoka katikati mwa jiji la Kampala.

Picha zilizosambazwa mitandaoni zilionyesha magari yakiteketea.

Hii ni mara ya tatu ndani ya muda wa miezi miwili kwa milipuko ya mabomu kutokea nchini Uganda.

Mwezi jana, watu wawili waliuawa na wengine kadha wakajeruhiwa katika mlipuko uliotokea katika mkahawa moja maarufu viungani mwa jiji la Kampala.

Ulitokea ndani ya mkahawa kwa jina Digida Eating Point ulioko eneo la Komamboga.

“Eneo la tukio limezingirwa na maafisa wa usalama kutoka kitengo cha kuchunguza mabomu wameitwa kuchunguza ikiwa mlipuko huo ni wa kimakusudi au la. Tunawashauri wananchi kuwa watulivu huku tukichunguza chanzo cha tukio hili,” msemaji wa polisi Fred Enanga akasema kupitia taarifa.

Mlipuko huo ulijiri baada ya mashirika kadha ya habari kuripoti kwamba Uingereza ilionya raia wake kuwa wafuasi wa kundi moja la kigaidi walikuwa wakipanga kushambulia Uganda.

Jumla ya watu 74 waliuawa katika shambulio la bomu lililotekelezwa na magaidi jijini Kampala mnamo Juni 12, 2010. Watu hao walikuwa miongoni mwa mamia ya mashabiki wa kandanda waliokuwa wakitizama mechi ya fainali ya Kombe la Dunia ndani ya klabu moja katikati mwa jiji hilo.

Milipuko ya jana imetokea siku chache kabla ya Rais wa Uganda Yoweri Museveni kuongoza mkutano wa marais wa mataifa ya ukanda wa Afrika Mashariki kujadili mapigano yanayoendelea nchini Ethiopia.

Rais Uhuru Kenyatta ni miongoni mwa viongozi walioalikwa katika mkutano huo ambao ulikuwa umeratibiwa kufanyika jijini Kampala.

Haikujulikana ikiwa mkutano huo bado utaendelea ulivyopangwa.

Mchakato wa kurejesha utulivu nchini Ethiopia ulishika kasi Alhamisi wiki jana baada ya mjumbe maalum wa Amerika anayesimamia Upembe mwa Afrika Jeffrey Feltman kuwasili nchini humo.

Rais Kenyatta pia alizuru taifa hilo ambapo alifanya mashauriano ya kina na Waziri Mkuu Abiy Ahmed.

You can share this post!

Kukubo angali na ndoto ya kuwa rais wa Kenya

Waandamanaji wapeleka maiti kwa ofisi ya serikali

T L