• Nairobi
  • Last Updated May 8th, 2024 8:50 AM
Dortmund yadhalilisha Wolfsburg

Dortmund yadhalilisha Wolfsburg

Na MASHIRIKA

BORUSSIA Dortmund walifunga mabao matano katika kipindi cha kwanza na kuzamisha chombo cha Wolfsburg kwa magoli 6-1 kwenye mchuano wa Ligi Kuu ya Ujerumani (Bundesliga).

Tom Rothe, Axel Witsel, Manuel Akanji, Emre Can na Erling Braut Haaland walitikisa nyavu za Wolfsburg katika dakika 45 za kwanza za pambano hilo kabla ya Haaland kufungia Dortmund bao la sita katika kipindi cha pili.

Ridle Baku alifuta machozi ya Wolfsburg dakika tisa kabla ya kipenga cha kuashiria mwisho wa mechi kupulizwa.

Dortmund kwa sasa wanashikilia nafasi ya pili kwenye msimamo wa jedwali la Bundesliga kwa alama 63, sita nyuma ya viongozi na mabingwa watetezi Bayern Munich.

Ni mara ya pili chini ya kipindi cha miezi miwili kwa Dortmund kufunga mabao sita katika mechi moja. Kikosi hicho kilinyuka Borussia Monchengladbach 6-0 ligini mnamo Februari 20, 2022.

Kichapo kutoka kwa Dortmund kilisaza Wolfsburg katika nafasi ya 13 kwenye jedwali la Bundesliga baada ya kupoteza mechi nne kati ya tano zilizopita huku wakifungwa mabao 14.

MATOKEO YA BUNDESLIGA (Jumamosi):

Dortmund 6-1 Wolfsburg

Mainz 0-0 Stuttgart

Augsburg 0-1 Hertha Berlin

Freiburg 3-0 Bochum

M’gladbach 1-3 Cologne

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Liverpool yadengua Man-City FA

Juventus na Bologna nguvu sawa

T L