• Nairobi
  • Last Updated May 8th, 2024 6:50 AM
Southampton yaendeleza masaibu ya Arsenal

Southampton yaendeleza masaibu ya Arsenal

Na MASHIRIKA

KOCHA Mikel Arteta amekiri kwamba kudorora kwa fomu ya kikosi chake cha Arsenal “kunazua hofu” baada ya kupokea kichapo cha 1-0 kutoka kwa Southampton mnamo Jumamosi uwanjani St Mary’s.

Mechi hiyo ilikuwa ya tatu mfululizo kwa Arsenal kupoteza katika kampeni za Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) msimu huu. Bao la pekee katika mchuano huo lilipachikwa wavuni na Jan Bednarek mwishoni mwa kipindi cha kwanza.

Bukayo Saka, Emile Smith Rowe na Martin Odegaard walipoteza nafasi nyingi za kufungia Arsenal licha ya kumtatiza pakubwa kipa Fraser Forster katika vipindi vyote viwili vya mchezo.

“Tumepoteza mechi kwa njia tofauti, lakini kupoteza pambano kwa namna tulivyofanya leo dhidi ya Southampton kunatia hofu na ni vigumu zaidi kuelezea,” akasema Arteta.

Matokeo hayo yalisaza Arsenal katika nafasi ya sita kwa alama 54 sawa na Manchester United waliotandika Norwich City 3-2. Ni pengo la alama tatu ambalo sasa linatamalaki kati ya Arsenal na Tottenham Hotspur ambao pia walicharazwa 1-0 na Brighton katika mchuano mwingine wa EPL mnamo Jumamosi.

Kwa upande wao, Southampton walichupa hadi nafasi ya 12 jedwalini kwa alama 39 sawa na Brentford. Ushindi dhidi ya Arsenal ulikuwa wao wa kwanza ligini tangu Februari 2022.

Arsenal walishuka dimbani wakitarajiwa kuweka kando maruerue ya kichapo cha 2-1 kutoka kwa Brighton mnamo Aprili 9, 2022 na kuweka hai matumaini ya kukamilisha kampeni za msimu huu ndani ya orodha ya nne-bora ili kufuzu kwa soka ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) muhula ujao.

Hadi waliposhuka dimbani kuvaana na Arsenal, Southampton walikuwa wamepoteza michuano mitano kati ya sita katika mashindano yote huku wakifungwa magoli 19, yakiwemo sita kutoka kwa Chelsea waliowaponda 6-0 katika mchuano wa awali. Aidha, walikuwa wameshinda mechi moja pekee kati ya 12 za awali dhidi ya Arsenal katika EPL.

Arsenal wangali na mtihani mgumu dhidi ya Tottenham Hotspur, Chelsea, Manchester United na West Ham katika mechi nne kati ya saba walizosalia nazo ligini muhula huu.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Brighton yazamisha Spurs

Kocha wa Bayern asema anatishiwa maisha baada ya kikosi...

T L